Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango amezindua maadhimisho ya wiki ya sheria leo tarehe tarehe 22 Januari, 2023 katika Viwanja vya Nyerere ‘Square’ jijini Dodoma.
Katika uzinduzi huo ambapo Mhe. Dkt. Mpango alikuwa mgeni rasmi wa shughuli hiyo amewataka watoa haki na washiriki wa maonesho hayo kuelimisha wananchi kuhusu njia bora za utatuzi wa migogoro hususani njia ya usuluhishi ambayo ina faida nyingi ikiwemo kuokoa muda, kupunguza mlundikano wa mashauri na kukuza uchumi wa Taifa.
Mhe. Dkt. Mpango aliendelea kwa kuwaomba Viongozi wa dini mbalmbali kuwakumbusha waumini wanawaongoza juu ya umuhimu wa utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi pia aliwahamasisha wananchi wote kutembelea Maonesho ya wiki ya sheria yanayoendelea nchi nzima ili kupata elimu inayotolewa na wadau hao wa utoaji haki.
Aidha, Mhe. Dkt. Mpango amewataka viongozi wa Mahakama kuzifanyia kazi changamoto kadhaa zilizopo katika Mahakama kwa baadhi ya watumishi ambao wanajihusisha na vitendo vya rushwa na ukiukwaji wa maadili pamoja na kuwawajibisha.
Kwa upande wake, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Mahakama ya Tanzania na Wadau wa utoaji haki kutumia maadhimisho ya wiki ya sheria kwa madhumuni ya kuwaelimisha wananchi ili kufahamu taratibu mbalimbali za kupata haki na kuwaelimisha juu ya haki na wajibu wao katika kupata haki.
Mhe. Prof. Juma pia alizungumzia suala la Usuluhishi kwa kusema wananchi wana wajibu wa kumaliza mashauri kwa njia ya usuluhishi na akatoa wito kwa wananchi kutembelea maonesho ya wiki ya sheria yanayotolewa maenneo mbalimbali nchi nzima.
Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ni miongoni mwa Wadau mbalimbali wa Mahakama, ambapo watashiriki katika Maadhimisho ya Wiki ya Sheria na wadau wengine wakiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Tume ya Haki za Binadamu, Chama cha Majaji na Mahakimu Wanawake (TAWJA), Polisi, Magereza na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS).
Katika maadhimisho haya ya Wiki ya Sheria na Siku ya Sheria, kauli mbiu itakuwa Umuhimu wa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya Usuluhishi Katika Kukuza Uchumi Endelevu: Wajibu wa Mahakama na Wadau.
Maonesho haya yaliyozinduliwa leo yatafanyika kwa muda wa siku nane ambapo yanatarajiwa kukamilika tarehe 29 Januari, 2023 ambapo yatahitimishwa kwa kilele cha Siku ya Sheria itakayofanyika tarehe 01 Februari, 2023 huku mgeni rasmi wa siku hiyo anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Makamu wa Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.
Philip Isdor Mpango akihutubia kwenye Maadhimisho ya Uzinduzi wa Wiki ya Sheria
yaliyofanyika leo tarehe 22 Januari, 2023 katika viwanja vya Nyerere Square
Jijini Dodoma.