Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma

Jaji kiongozi wa Tanzania

Mhe. Profesa Ibrahim Hamis Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania (katikakati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wahitimu wa stashahada ya sheria

Mahafali ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto yaliyofanyia 18 Desemba, 2020

Mahafali ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto yaliyofanyia 18 Desemba, 2020

Monday, November 29, 2021

CHUO CHA UONGOZI WA MAHAKAMA LUSHOTO CHAPONGEZWA KUWA NI KISIMA CHA UTOAJI MAFUNZO KWA WATUMISHI WA MAHAKAMA

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani leo tarehe 29 Novemba, 2021 amefungua mafunzo elekezi ya siku tano kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama ambapo amekisisifia Chuo cha Uongozi wa  Mahakama Lushoto (IJA) kwa mchango mkubwa kinachofanya na kujenga  taaluma  bora kwa watumishi wa Mahakama na wananchi wengine kwa ujumla.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo ya siku tano yanayowashirikisha viongozi hao, Mhe. Siyani amebainisha kuwa Chuo kwa kushirikiana na Kitengo cha mafunzo cha Mahakama ya Tanzania wamekuwa wakifanya kazi nzuri kwa kutoa mafunzo mbalimbali elekezi na endelevu kwa watumishi wa Mahakama ya Tanzania.

 “Kama ilivyo kwa wengine, mimi nina imani kuwa chuo hiki kweli ni kitovu na kisima cha elimu bora. Kimsingi, chuo hili kina uwezo wa kujenga  taaluma  na kufanya leo hii tuna Wasajili  ambao kesho ni Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania. Kwa hiyo, mimi niwapongeze sana na nifikishie salamu zangu kwa Mkuu wa Chuo,” Jaji Kiongozi alimweleza Kaimu Mkuu wa Chuo, Prof. Fatihiya Massawe, ambaye pia ni Naibu Mkuu wa IJA, Mipango, Fedha na Utawala.

Amesema kuwa mafanikio katika utoaji wa mafunzo elekezi ya awali na mafunzo endelevu ya kimahakama ni mojawapo ya matunda ya kazi nzuri yanayofanywa na IJA kwa kuzingatia Sera ya Mafunzo ya Mahakama ya mwaka 2019 ambayo inakitambua Chuo hicho kama kitovu au kisima cha utoaji mafunzo kwa watumishi wa Mahakama, lakini vile vile utafiti wenye lengo la kuongeza tija na kuboresha utendaji wa Mahakama ya Tanzania.

Jaji Kiongozi aliwakumbusha washiriki kuwa mafunzo ambayo yameandaliwa kwa ajili yao yamelenga kuwapa mbinu na nyenzo sahihi za kuweza kukabili changamoto mbalimbali za kiutendaji. “Hivyo muwe wazi kuuliza maswali na kuchangia uzoefu kila mmoja kwa namna ambayo mnaona italeta matokeo chanya katika utendaji kazi wenu. Shabaha ya kila mmoja wetu iwe ni utoaji wa haki na kuliletea maendeleo taifa letu na kutekeleza kwa vitendo Mkataba wa Huduma kwa Mteja,” amesema.

Mhe. Siyani alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha washiriki wa mafunzo hayo kuwa wapo katika kipindi cha mapinduzi ya nne ya viwanda na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amekuwa akisisitiza watumishi wa Mahakama kujinoa zaidi kwenye eneo la TEHAMA ili waweze kuendana na kasi ya mabadiliko ya kidunia hivi sasa.

Amebainisha kuwa miongoni mwa mada zitakazotolewa katika mafunzo hayo inahusu TEHAMA, hivyo ni imani yake kupitia mada hiyo washiriki wote watapata nafasi ya kujifunza juu ya nafazi zao katika usimamizi wa mashauri kwa njia za kielektroniki. Aliwaomba kutumia fursa hiyo kupata kitu cha nyongeza katika eneo hilo na kwamba kila mmoja wao awe mfuasi wa karibu wa TEHAMA kama dunia inavyowataka hivi sasa.

“Tambueni kwamba tunakoelekea hakutakuwa na nafasi kwa Msajili au Mtendaji asiye na uelewa wa TEHAMA katika Mahakama yetu. Hiyo ni dhahiri kwa sababu ninyi ni wasimamizi wa mifumo ikiwemo ya TEHEMA na bila shaka msimamizi bora ni yule anayefahamu anachokisimamia,” aliwaambia viongozi hao wa Mahakama ya Tanzania.

Awali akitoa neno la ukaribisho, Kaimu Mkuu wa Chuo, Prof. Fatihiya Massawe alisema kuwa mafunzo yanayotolewa kwa Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama siyo ya kwanza kutolewa hapo Chuoni, kwani IJA imekuwa ikitoa mafunzo elekezi (Induction) kwa wahesimiwa Majaji wote wapya wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na mafunzo ya awali na elekezi kwa Majaji wote wapya wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Zanzibar wanapoteuliwa kwenye wadhifa huo na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani pamoja na Rais wa Zanzibar.

Kwa mujibu wa Prof. Massawe, vilevile IJA imekuwa ikiendesha mafunzo elekezi kwa Mahakimu wote mara wanapoajiriwa kujiunga kwa mara ya kwanza na utumishi wa Mahakama kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kutenda haki kwa wote na kwa wakati kwa kuzingatia misingi ya sheria na uadilifu.

“Hii ni mara ya kwanza mafunzo ya namna hii yametolewa kwa Naibu Wasajili na hata kwa Watendaji. Tunapenda kuipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kulisimamia hili. Tunaamini mafunzo haya elekezi ni mwanzo tu wa mafunzo endelevu ambayo washiriki hawa wataendelea kupata kama watumishi wa Mahakama. Chuo kinaahidi kitaendelea kutayarisha programu za mafunzo kulingana na uhitaji kadri watakavyoendelea kutekeleza majukumu yao na kubaini changamoto katika maeneo ya uhitaji wa mafunzo,” alisema.

Katika mafunzo hayo, mada mbalimbali zitawasilishwa na waezeshaji waliobobea katika maeneo mbalimbali, akiwemo Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Wilbert Chuma, Jaji Mkuu Mstaafu ,Mohamed Chande Othman, Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Mhe. January Msoffe, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Katarina Revocati na watendaji wengine waandamizi wa Mahakama.

Miongoni mwa mada zitakazowasilishwa kwenye mafunzo hayo zinajumuisha Uongozi wa Kimkakati, Stadi za Uongozi na Uwezo wa Kukabili Mabadiliko, Wajibu wa Mahakama, Utamaduni wake na Uhusiano wake na Mihimili Mingine ya Dola, Sheria ya Uendeshaji wa Mahakama na Uboreshaji unaofanywa na Mahakama, Maadili ya Watumishi wa Umma na Maadili ya Kimahakama, Usimamizi wa fedha na Manunuzi ya Umma pamoja na Usimamizi wa Nyaraka.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani akifungua mafunzo elekezi kwa Naibu Wasajiri na Watendaji wa Mahakama yanayofanyika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.


Kaimu Mkuu wa Chuo, Prof. Fatihiya Massawe, ambaye pia ni Naibu Mkuu wa IJA, Mipango, Fedha na Utawala akitoa neno la ukaribisho kabla ya ufunguzi wa mafunzo ya siku tano yanayowashirikisha Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama ambayo yanafanyika katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA). ,Mafunzo hayo yamefunguliwa leo tarehe 29 Novemba, 2021 na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani.



Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akisistiza jambo alipokuwa anatoa mada katika mafunzo hayo.

 

Sehemu ya Naibu Wasajili na Watendaji wa Mahakama ya Tanzania (juu na picha za chini) wakifuatilia mada iliyokuwa inatolewa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.








 


 


 

 

 


 


 

 

Wednesday, November 17, 2021

MAFUNZO KWA WAWEZESHAJI WA MAFUNZO YA MASHAURI YA MTOTO

Mhe. Dkt Paul F. Kihwelo, Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama leo amefungua rasmi mafunzo kwa wawezeshaji 36 wa mafunzo ya haki za watoto kutoka sehemu mbalimbali Tanzania. Mafunzo haya yanafanyika kwa muda wa siku tano kuanzia tarehe 15 Novemba mpaka 19 Novemba katika ukumbi wa St. Gaspar jijini Dodoma. Mafunzo hayo yameandaliwa na Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) chini ya ufadhili wa Shirika linalohudumia watoto duniani (UNICEF). 
Washiriki wa mafunzo haya ni Majaji kutoka Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu, Mahakimu wakazi wa ngazi mbalimbali, Waendesha Mashtaka na Maafisa Ustawi wa Jamii. Washiriki hawa watapitishwa katika mada mbalimbali zitakazowawezesha kuwa na uelewa na ujuzi wa pamoja juu ya uendeshaji bora wa mashauri ya mtoto. 

Katika mafunzo haya kutakuwa na mada mbalimbali zitawasilishwa na wawezeshaji mahiri na wabobezi katika masuala ya namna bora ya uendeshaji wamashauri hayo ambao ni Mhe. Sophia Wambura Jaji Mstaafu na Mhe. Matilda Philip Wakili Mstaafu wa kujitegemea. Akiongea katika ufunguzi wa mafunzo haya Mhe. Dkt. Kihwelo aliezea lengo kubwa la mafunzo haya kuwa ni kuwajengea uwezo wadau wanaoendesha mashauri ya mtoto. Kundi hilo linalofundishwa mafunzo hayo pia ni kwa ajili ya kuwaandaa ili waweze kufundisha wengine kwenye masuala ya haki za mtoto anapokuwa mhanga. Hii imekuja kwa ajili ya kuongeza kundi la wawezeshaji baada ya wengi waliofanya mafunzo ya namna hii kustaafu. 

Kwa upande wake mwakilishi kutoka UNICEF, Bi. Victoria Mgonela ameushukuru uongozi wa mahakama na Chuo kwa kulipa uzito wa kipekee suala la uendeshaji wa mashauri ya mtoto na kuahidi kuwa UNICEF itaendelea na mashirikiano hayo.

Mafunzo kama hayo yalishawahi kuendeshwa mwaka 2014 ambapo ilijumuisha majaji 6, Mahakimu wakazi 6, maafisa ustawi wa jamii 2 na watumishi 3 kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.
Mhe. Dkt Paul F. Kihwelo Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania akifungua mafunzo kwa wawezeshaji wa mafunzo ya haki za watoto mafunzo yatafanyika katika ukumbi yanayofanyika katika ukumbi wa St. Gasper jijini Dodoma
Bi. Victoria Mgonela Mwakilishi wa UNICEF akitoa salamu kutoka Shirika la UNICEF nchini Tanzania kwenye ufunguzi wa mafunzo hayo yanayofanyika katika ukumbi wa St. Gasper jijini Dodoma
Picha ya pamoja ya Majaji wanaoshiriki katika mafunzo ambao ni Mhe. Rehema Sameji, Jaji wa Mahakama ya Rufani (katikati), Mhe. Paul Kihwelo, Jaji wa Mahakama ya Rufani (wa pili kushoto) na Mhe. Issa Maige, Jaji wa Mahakama ya Rufani (wa pili kulia). Wengine ni Mhe. Devotha Kamuzora, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania (wa kwanza kushoto na Mhe. John Chaba, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania (wa kwanza kulia).
Majaji wanaoshiriki katika mafunzo (ambao wamekaa) wakiwa katika picha ya pamoja na washiriki.
Majaji wanaoshiriki katika mafunzo (ambao wamekaa) wakiwa katika picha ya pamoja na washiriki.
Majaji wanaoshiriki katika mafunzo (ambao wamekaa) wakiwa katika picha ya pamoja na sekretarieti kutoka IJA.
Baadhi ya Washiriki wa mafunzo kwa wawezeshaji wa mafunzo ya haki za watoto wakiwa wanasikiliza mada zinazoendelea katika mafunzo hayo kutoka kwa muwezeshaji Mhe. Sophia Wambura Jaji Mstaafu (hayupo pichani)

Saturday, November 13, 2021

MAHAFALI YA 21 YA CHUO CHA UONGOZI WA MAHAKAMA LUSHOTO


WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA ATAMBUA MCHANGO WA CHUO CHA UONGOZI WA MAHAKAMA LUSHOTO KATIKA KUTOA MAFUNZO KWA WADAU WA UTOAJI HAKI NCHINI. 

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Prof. Palamagamba J.A.M. Kabudi ametambua mchango wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama- Lushoto katika kutoa mafunzo ya utoaji haki nchini.

Waziri Kabudi ameongea hayo alipokuwa akihutubia kwenye mahafali ya Ishirini na Moja ya Chuo hicho yaliyofanyika tarehe 12 Novemba, 2021 Chuoni Lushoto.

Waziri Kabudi alisisitiza kuwa umuhimu wa Chuo kuwa kitovu cha kutoa mafunzo sio tu kwa Mhimili wa Mahakama, bali pia kwa Taasisi za Umma zinazohitaji elimu endelevu inayolenga kuboresha utoaji haki na usawa katika jamii.

Waziri Kabudi amewaomba wahitimu katika mahafali hayo kutumia hatua waliyofikia kuwa chachu ya kujiendeleza zaidi kwenye elimu kwani ulimwengu wa sasa unahitaji zaidi watu wenye ujuzi na maarifa ya kutosha.

Waziri Kabudi aliendelea kwa kusema kuwa tangu kuanzishwa kwa Chuo hicho, mhimili wa Mahakama ndiyo mnufaika mkubwa wa zao la kitaaluma la Chuo hicho kwani mhimili huu umeweza kuendeleza watumishi wake pamoja na kuajiri mahakimu na watumishi wengine kutoka katika Chuo hiki. Aliongeza kwa kusema pamoja na hayo yote Chuo pia kimekuwa kikiratibu na kufanya mafunzo endelevu ya kujengea uwezo watumishi mbalimbali wa mahakama.

Waziri Kabudi aliongeoza maandamano na kutunuku stashahada na astashahada kwa wahitimu wa Chuo hicho pamoja na kutaja mambo sita ambayo yameipaisha Tanzania duniani  na kuibuka kuwa nchi ya mfano wa kuigwa inapoelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 60 ya uhuru wake.

Mambo yaliyotajwa na Waziri Kabudi ni pamoja na misingi iliyoachwa na baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ya kuondoa ukabila nchini na kuifanya Tanzania kuwa taifa badala ya mkusanyiko wa makabila, taifa kuingia katika uchumi wa kati kabla ya muda uliotazamiwa yaani mwaka 2025, uwezo wa taifa kudumisha na kuenzi tunu ambazo ni amani,umoja,mshikamano,utu,haki,heshima ya mwanadamu, uhuru na demokrasia. Mambo mengine aliyotaja Waziri ni uthubutu wanchi yetu kuendesha miradi mikubwa kwa kutumia rasilimali na fedha zake za  ndani, uwezo wa taifa kuzifanya rasilimali zilizokuwa za Watanzania ikiwemo kuvunja mikataba mibovu ambayo haikuwa na tija kwa taifa na jambo la mwisho lililotajwa na Mhe. Prof. Kabudi ni ukomavu wa kisiasa na ukatiba katika taifa letu.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mheshimiwa Dkt. Gerald A. M. Ndika amesema Chuo kimekabidhiwa majukumu ambayo ni kutoa mafunzo, kufanya tafiti na kutoa huduma za kitaalamu majukumu ambayo Chuo kinamudu kuyatekeleza kwa ufanisi.

“Sera ya mafunzo ya mahakama ya mwaka 2019 imebainisha kuwa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto  ni kitovu na wakala wa mafunzo na utafiti wa Mahakama Tanzania na kutokana na hilo tumeendelea kuboresha utendaji kazi wa Chuo ikiwemo kurugenzi ya mafunzo endelevu ya kimahakama” amesema Dkt. Ndika.

Kwa upande wake, Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo Mhe. Dkt. Paul Kihwelo ametaja changamoto zinazokikabili Chuo ikiwepo ufinyu wa bajeti,kutopewa kibali cha kuajiri, uchakavu wa miundombinu na uchache wa mabweni ya wanachuo.

Mkuu huyo wa Chuo aliendelea kwa kusema kuwa uchakavu wa miundombinu unatokana na majengo ya chuo kuwa makongwe ambapo yanalazimika kukarabatiwa ili kutumika kwa usalama.

Hata hivyo Mhe. Dkt. Kihwelo alieleza kwamba pamoja na changamoto zilizopo Chuo kimeendelea kufanya majukumu yake ya kitaaluma kama Chuo kilivyokusudiwa kuyafanya. Na pia aliupongeza uongozi mzima wa Mahakama ya Tanzania kwa kukiamini Chuo.

Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Prof. Palamagamba J.A.M. Kabudi akihutubia kwenye mahafali ya 21 ya wahitimu wa Stashahada na astashahada ya sheria wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi akiongoza Maandamano kabla ya kuanza kwa sherehe za Mahafali ya 21 ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto leo wilayani Lushoto, Tanga. Waziri Kabudi alikuwa Mgeni rasmi kwenye Mahafali hayo. Kulia ni Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo hicho, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Gerald


Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Prof. Palamagamba J.A.M. Kabudi akiwa katika picha ya pamoja na wahitimu wa astashahada ya Sheria waliofanya vizuri kitaaluma katika masomo yao wakati wa mahafali ya 21 ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto


Wahitimu wakitunukiwa Stashahada ya Sheria katika Mahafali ya 21 ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto leo wilayani Lushoto, Tanga. Waziri Kabudi alikuwa Mgeni rasmi kwenye Mahafali hayo.

Wahitimu wakitunukiwa Astashahada ya Sheria katika Mahafali ya 21 ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto leo wilayani Lushoto, Tanga. Waziri Kabudi alikuwa Mgeni rasmi kwenye Mahafali hayo.

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul Kihwelo akizungumza wakati wa sherehe hizo.

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Baraza la Uongozi wa Chuo hicho.

Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na wanachama wa chama cha wanafunzi waliowahi kusoma katika chuo hicho. 


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wahitimu wa Astashahada ya Sheria. 

Mmoja wa Wahitimu wa Stashahada ya Sheria ambaye ni mshindi wa masomo kadhaa akipokea zawadi ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma aliyotoa kwa washindi wote katika masomo.

Wednesday, November 10, 2021

ZIARA YA MAKAMISHINA WA TUME YA UTUMISHI WA MAHAKAMA

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel ameahidi kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ili kiweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu, ikiwemo kutoa wahitimu bora watakaolisaidia taifa katika maeneo mbalimbali ya maendeleo.

Prof. Ole Gabriel, ambaye ni Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama alitoa ahadi hiyo katika ziara ya Tume iliyofanya katika Chuo hicho hivi karibuni kutembelea maeneo mbalimbali, likiwemo Jengo la Hostel ya Wavulana ambalo linajengwa kwa kugharamiwa na Mahakama ya Tanzania katika mpango wa uboreshaji wa majengo chuoni hapo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la Chuo, Mhe. Dkt. Gerald Ndika, ambaye ni Jaji wa Mahakama ya Rufani aliupongeza uongozi wa Chuo kwa jitihada zake inazozifanya katika kutoa mafunzo yanayolenga kuwajengea uwezo watumishi mbalimbali wa Mahakama ya Tanzania.

Katika ziara hiyo, ambayo ni mwendelezo wa shughuli mbalimbali zinazofanyika kuelekea siku ya mahafali ya ishirini na moja ambayo inafanyika tarehe 12 Novemba, 2021, Prof. Ole Gabriel ameambatana na Makamishna mbalimbali wa Tume ya Utumishi wa Mahakama.

Wajumbe wa Tume hiyo pia walipata nafasi ya kukutana na menejimenti ya Chuo ambapo walifanya majadiliano yaliyolenga kuboresha huduma zinazotolewa na chuo hicho. Katika kikao hicho, Katibu wa Tume hiyo ambaye ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama alitoa salamu kwa niaba ya wajumbe wa Tume hiyo.

Prof. Elisante aliiambia Menejimenti kwamba Chuo kina wajibu mkubwa kwa Mahakama ya Tanzania na Taifa kwa ujumla katika kutoa elimu ambayo italeta matokeo chanya kwa taifa sio tu kwa kufaulu katika mitihani mbalimbali bali kutoa wanafunzi waliobora ambao wanaweza kufanya kazi popote na katika mazingira yoyote.


Mhe. Dkt Paul Kihwelo akiwa na Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama akipitishwa katika maeneo mbalimbali ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto wakati wa ziara ya siku moja 
Wajumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama wakipata maelezo kuhusu jengo la bweni la wavulana ambalo linajengwa kwa kupitia fedha za mahakama ya Tanzania  kutoka kwa Afisa Miliki wa Chuo Bwana George Masanja 


Wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Mahakama wakiwa katika picha ya pamoja na wanachuo wa Stashahada ya Sheria mwaka wa pili walipotembelea hivi karibuni katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto

Wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Mahakama, Baraza la Uongozi wa Chuo wakiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya Chuo walipokuwa kwenye ziara ya siku moja chuoni hapo hivi karibuni
Wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Mahakama na  Baraza la Uongozi wa Chuo wakiwa katika picha ya pamoja na  Sekretarieti ya Tume ya Utumishi wa Mahakama walipokuwa kwenye ziara ya siku moja chuoni hapo hivi karibuni
Wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Mahakama na  Baraza la Uongozi wa Chuo wakiwa katika picha ya pamoja na  Sekretarieti ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto walipokuwa kwenye ziara ya siku moja chuoni hapo hivi karibuni