Na Rosena Suka, IJA
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo leo tarehe 25 Novemba, 2022 amefungua mafunzo elekezi ya siku moja kwa Viongozi wa Serikali ya Wanachuo wa IJA (IJASO) yaliyofanyika Chuoni Lushoto.
Katika ufunguzi huo Mkuu wa Chuo amewaeleza viongozi hao kwamba wanawajibu mkubwa wa kuwahudumia kwa
uadilifu wanachuo wenzao kwani wao ni kiungo
katika kufikisha yale ambayo yanatoka kwenye
Uongozi wa Chuo kwenda kwa wanachuo na kutoka kwa wanachuo kwenda kwenye Uongozi
wa Chuo.
Mkuu wa Chuo
aliwasisitiza viongozi hao wa wanachuo kutumia vikao mbalimbali watakavyokuwa
navyo ili kutatua changamoto zao na sio kulalamika au kupeleka changamoto zao kwenye
mamlaka zisizohusika. Aliendelea kwa kuwataka viongozi hao kusimamia sheria,
kanuni na taratibu zilizopo ili kuonyesha mfano bora kwa wanachuo wenzao,
Mkuu wa Chuo,
aliwakumbusha viongozi hao kuwa na ushirikiano kati ya wao wenyewe, watumishi
wa Chuo na wanachuo wenzao bila kusahau
mahusiano mazuri na jamii inayowazunguka.
Kwa upande wake Rais wa
Wanachuo, Bw. Meshack D. Tupa alipokuwa akitoa shukrani zake ameushukuru Uongozi
wa Chuo kwa kuandaa na kuwapatia semina hiyo elekezi na kuahidi kufanya kazi
kwa ushirikiano na watumishi wa Chuo na wanachuo wanaowawakilisha.
Viongozi hawa wa
wanafunzi katika semina hiyo elekezi wamepitisha katika mada mbalimbali ambazo
ni Masuala ya Usalama na Maadili, Unyanyasaji na Ukatili wa Kijinsia, Uongozi
na Taaluma, Usimamizi wa Rasilimali za IJASO na Usitawi wa Wanachuo.
IJA imekuwa na utaratibu
wa kutoa mafunzo elekezi kwa Serikali ya Wanachuo mara tu inapowekwa
madarakani.
Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi Mahakama Lushoto, Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo akihutubia Viongozi wa Serikali ya Wanafunzi wakati wa ufunguzi wa Mafunzo Elekezi ya siku moja yaliyofanyika Chuoni Lushoto