Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma

Jaji kiongozi wa Tanzania

Mhe. Profesa Ibrahim Hamis Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania (katikakati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wahitimu wa stashahada ya sheria

Mahafali ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto yaliyofanyia 18 Desemba, 2020

Mahafali ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto yaliyofanyia 18 Desemba, 2020

Monday, March 21, 2022

WANAWAKE IJA WAADHIMISHA SIKU YA WANAWAKE KWA KUTEMBELEA WAFUNGWA

Watumishi wanawake wa Chuo cha uongozi wa Mahakama Lushoto katika kuadhimisha siku ya wanawake duniani kama ilivyo ada, mapema leo machi 8, 2022 wametembelea wafungwa wa Gereza la Wilaya ya Lushoto na kutoa msaada wa mahitaji ya kibinadamu wa vifaa mbalimbali vikiwemo taulo za usafi kwa Wanawake, Sabuni za kufulia na kuogea, dawa za meno na miswaki, mafuta ya kupaka na dawa za mbu.

 Akikabidhi msaada huo, mwenyekiti wa watumishi wanawake wa chuo alisema kuwa, lengo la kwenda gerezani hapo ni kuwafariji na kuwatia moyo ili wasikate tamaa kwani hakuna binaadamu aliye mkamilifu hivyo na kuongeza kuwa, pamoja na kuwa wako katika kutumikia adhabu zao ni vyema kuwakumbuka na kuwakumbusha kuwa wao ni sehemu ya jamii na inawathamini kama walivyo binaadamu wengine.


Baada ya zoezi la kutembelea wafungwa, wanawake wa IJA walipata nafasi ya kukaa pamoja na Uongozi wa Chuo kwenye tafrija fupi iliyoandaliwa na Chuo kwenye hotel ya Mullers Lodge iliyoko Wilayani Lushoto.  Akitoa salamu kwa niaba ya Mkuu wa Chuo kwenye ufunguzi wa tafrija hiyo, Mhadhiri Dkt. Ismail Hokororo aliwapongeza wanawake hao kwa kujitokeza na kuenzi maadhimisho ya siku ya Wanawake na kusema kuwa Chuo kinatambua na kuthamini  mchango wa Mwanamke katika jamii na  kipo  tayari kuwasikiliza na kutoa ushirikiano unaostahili pale utakapohitajika  na kuwahakikishia mazingira mazuri ya kufanya kazi yanayozingatia usawa kwa maendeleo ya mwanamke.


Dkt. Hokororo aliendelea kusema kuwa Menejimenti ya Chuo inaunga mkono jitihada zote zinazoibuliwa na wanawake zinazolenga kujenga umoja, uzalendo, mshikamano kwa ustawi wa chuo na Taifa kwa ujumla.

“Nyote ni mashahidi wa jitihada zinazoendelea katika kuboresha uwiano wa kiutumishi kwa wanawake na wanaume chuoni, hasa katika maeneo yale yaliyo chini ya mamlaka ya Menejimenti ya Chuo” alisema Dkt. Hokororo.


Dkt. Hokororo aliwatia moyo wanawake hao kuendelea kushirikiana na kubadilisha uzoefu huku wakiandaa mipango endelevu kwa mustakabali wa Maendeleo ya Wanawake na jamii kwa ujumla.

Katika kuadhimisha siku hiyo pia wanawake wa IJA walipitishwa kwenye mada mbili ambazo ziliandaliwa na Chuo kwa ajili ya kuwapa uelewa zaidi juu ya masuala ya siku ya wanawake ambazo zilikuwa ni mada ya Nafasi ya Mwanamme katika kumkomboa mwanamke na mada ya pili iliyohusu Umuhimu wa Wanawake Kujiunga Pamoja.

 

Maadhimisho ya siku ya wanawake duniani hufanyika Machi 8 kila mwaka, kiwilaya maadhismisho haya yamefanyika katika kijiji cha Gare ambapo viongozi mbalimbali walihudhuria na kutoa salamau zao kuhusu masuala mbalimbali ya haki na usawa kwa jinsia na pia kusisitiza juu ya umuhimu wa kuhesabiwa sambamba na dhima ya mwaka huu isemayoKizazi cha Haki na Usawa kwa Maendeleo Endelevu: Tujitokeze kuhesabiwa’’. Dhima hii inaenda sambamba na mpango wa serikali wa kuendesha zoezi la sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika mwezi septemba, 2022 nchini.


Dkt. Joseph Hokororo Ismail, Mhadhiri wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto akitoa Salamu za Siku ya wanawake kwa niaba ya Mkuu wa Chuo, pembeni kwake ni Mwenyekiti wa watumshi wanawake wa Chuo Bi. Mariamu George.


Picha ya pamoja ya baadhi ya watumishi wanawake wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto waliohudhuria kwenye tafrija fupi iliyoandaliwa na Uongozi wa Chuo kwa ajili ya maadhimisho ya siku ya wanawake ulimwenguni.


PICHA ZA CHINI NI PICHA MBALIMBALI ZA MATUKIO YA SIKU YA WANAWAKE 









Wednesday, March 16, 2022

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA KATIBA NA SHERIA ZIARANI IJA

Na: Rosena Suka IJA Lushoto

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wamefanya  ziara ya kukagua mradi wa ujenzi wa bweni la ghorofa nne la wavulana lenye thamani ya shilingi za kitanzania billioni 2.64  lenye uwezo wa kulaza wanachuo 320. Mradi huu unasimamiwa na Mahakama ya Tanzania katika mpango wa Maboresho ya Mahakama.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa jengo hilo la bweni la wavulana Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel ametoa ufafanuzi wa ujenzi wa jengo hilo kuwa umefanyika katika awamu tatu tofauti ambazo zilisimamiwa na wakandarasi watu watatu kwa nyakati tofauti toka kuanza kwa mradi wa ujenzi huo mwaka 2011.  

Prof. Elisante alitoa maelezo hayo kwa kusema kuwa awamu ya kwanza ya mradi huo ilikuwa chini ya mkandarasi Beijini Construction Engineering Group ambaye alijenga kuanzia msingi hadi boma. Hatua ya pili ilikuwa ni uwekaji wa mifumo mbalimbli katika jengo hilo chini ya usimamizi wa Mkandarasi Froton Afrika Limited na Mkandarasi aliyepo kwa sasa ni  MS-Works Construction Limited ambaye anaendelea na umaliziaji wa jengo hilo  ambalo litakapokamilika litakuwa na       miundombinu ambayo itawezesha wanafunzi kutoka katika makundi maalum kulitumia.

Pamoja na mengine Prof. Elisante alimalizia kwa kusema kuwa, jengo hilo litakabidhiwa ifikapo Mei, 2022 na linatarajiwa kutumiwa na wanachuo watakaosajiliwa katika mwaka wa masomo 2022/2023 ambapo litapunguza idadi kubwa ya wanachuo wakiume wanaoishi nje ya mazingira ya Chuo.

Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Tabora Mjini Mhe. Emmanuel Mwakasaka ameipongeza Serikali kwa hatua iliyofikia ya ukamilishwaji wa ujenzi wa Jengo la Bweni la Wavulana la Chuo cha Uongozi wa Mahakama. Hatua ya ujenzi wa bweni hili litakuwa ni mkombozi kwa Chuo kwani litawezesha wanachuo kuweza kuishi ndani ya chuo badala ya kuchanganyika na wenyeji.

“Miradi ya ujenzi wa majengo haya imeenda kwa haraka sana na tumeridhishwa sana na kazi iliyofanyika, pongezi kwa watendaji wote wa Mahakama”, alisema Mhe. Mwakasaka.

Naye, Naibu Waziri, Wizara ya Katiba na Sheria Mhe. Geogrey Pinda (MB) alishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa kutembelea mradi huo na kuahidi kuwa hoja zote zilizotolewa na wajumbe zimepokelewa na zitafanyiwa kazi. Mhe. Pinda pia alitoa mapendekezo kwa Chuo kutumia nafasi waliyonayo kuendelea kuwajengea uwezo watumishi wa mahakama ili kusaidia mabadiliko ya mahakama kwenda sambamba na wataalamu.

Kwa upande wake Naibu Mkuu wa Chuo Taaluma, Tafiti na Ushauri Bw. Goodluck Chuwa ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kutoa ushirikiano mkubwa kwa Chuo kwa kukiwezesha mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi wa kada mbalimbali wa Mahakama pamoja na wadau wa sheria nchini.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria imefanya  ziara ya siku moja ambapo imekagua mradi wa ujenzi wa jengo la bweni la wavulana la Chuo cha Uongozi Mahakama Lushoto  ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya kamati hiyo ikiwemo kufanya ukaguzi wa miradi ya ujenzi inayosimamiwa na Mahakama ya Tanzania.




Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa maelezo mafupi juu ya ujenzi wa bweni la wavulana kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria na viongozi wengi wa Wilaya waliohudhuria katika tukio hilo.



Meza Kuu katika picha ya pamoja naWajumbe waKamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria
Picha ya juu na chini ni mwonekano wa nje na wa ndani wa bweni la wavulana ambalo lipo katika hatua ya ujenzi.

(Picha na Ibrahim Mdachi - IJA Lushoto)