Mafunzo hayo ya siku tano ni mtiririko wa mafunzo mengine kama hayo yaliyofanyika
jijini Arusha kuanzia tarehe 10 hadi 14 Oktoba 2022 kwa kundi la kwanza lililojumuisha
Majaji wa Mahakama Kuu, Waendesha Mashtaka Waandamizi na Wapelelezi Waandamizi,
na kufuatiwa na kundi la pili la mahakimu,
waendesha mashtaka na wapelelezi kuanzia tarehe 17 hadi 21 Oktoba 2022. Hili ni
kundi la tatu na mwisho ambalo linashiriki mafunzo hayo katika Chuo cha Uongozi
wa Mahakama Lushoto ambayo yanahitimishwa.
Akiongea wakati wa ufunguzi Mhe. Latifa Mansour alieleza kuwa mafunzo
haya yana lengo la kuwaleta pamoja wadau wa utoaji haki jinai na kubadilishana
uzoefu kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo sheria za kimataifa na kitaifa za
wanyamapori na misitu ikiwemo upelelezi
na uendeshaji wa mashauri ya makosa dhidi ya wanyamapori na makosa yanayohusiana
na hayo.
Aidha, Mhe. Mansour aliongeza kwa kusema kuwa mafunzo haya
yatawawezesha wapelelezi namna ya kufanya upelelezi kama sheria inavyotaka ili
kuwezesha kesi za namna hiyo zinapofikishwa Mahakamani na waendesha mashitaka ziwe
na ushahidi wa kutosha na kutokutoa mwanya kwa mtu aliyefanya kosa kukwepa kwa
visingizio mbalimbali.
“Tunaamini kwamba kama Mahakama pamoja na upelelezi itashirikiana na kuhakikisha kwamba hawa watakaobainika na makosa hayo watachukuliwa hatua zipasazo na wanapata adhabu za kutosha ili iwe funzo kwa jamii yote na wale wote wanaofanya biashara hizi haramu.” Alisema Jaji huyo.
Naye mwakilishi wa PAMS Foundation, Bw. Samson Kassala alieleza
kuwa Taasisi hiyo isiyo ya
kiserikali inajishughulisha na masuala ya uhifadhi wa mazingira na usalama wa wanyamapori.
Makao Makuu ya Taasisi hiyo yako jijini Arusha. Bw.
Kassala alifafanua kwa kusema PAMS Foundation imekuwa ikisaidia katika kuwajengea
uwezo wale wote walio mstari wa mbele katika kulinda ulinzi wa maliasili zetu kwa manufaa ya wananchi
na vizazi vijavyo kama sheria za nchi zinavyosema.
Bw. Kassala aliendelea kwa kusema kuwa PAMS Foundation imeendelea kushirikiana na Serikali na wanafanya hivyo ili kuunga mkono juhudi za Serikali ya Tanzania kwenye maeneo mengi ikiwemo utalii na hasa baada ya ziara ya Utalii (Royal Tour) ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Mafunzo hayo ni sehemu ya
utekelezaji wa makubaliano kati ya IJA na PAMS Foundation ambayo yalisainiwa
tarehe 23/06/2022 jijini Dar es Salaam kati ya Mkuu wa Chuo pamoja na
Mkurugenzi Mtendaji wa PAMS Foundation.
Picha mbalimbali za washiriki wa mafunzo ya uendeshaji wa mashauri ya makosa dhidi ya wanyamapori yanayofanyika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) wakiwafuatilia hotuba ya Mgeni rasmi wakati wa ufunguzi.