Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma

Jaji kiongozi wa Tanzania

Mhe. Profesa Ibrahim Hamis Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania (katikakati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wahitimu wa stashahada ya sheria

Mahafali ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto yaliyofanyia 18 Desemba, 2020

Mahafali ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto yaliyofanyia 18 Desemba, 2020

Wednesday, May 25, 2022

JAJI MKUU WA UGANDA AFANYA ZIARA IJA

Jaji Mkuu wa Uganda, Mhe. Alfonse Chigamoy Owiny-Dollo leo tarehe 25 Mei, 2022 amefanya ziara ya kutembelea Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na kujionea shughuli mbalimbali zinafanywa na Chuo.

 

Katika ziara yake, Mhe. Owiny-Dollo ameambatana na Maafisa 12 kutoka nchini Uganda ambao  miongoni mwa aliombatana nao ni Jaji Kiongozi wa Uganda Mhe. Dkt. Flavian Zeija, Msajili ya Mahakama ya Uganda, Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa JTI Uganda, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya JTI Uganda, Msajili waTaasisi ya JTI Uganda na viongozi wa International Development Law Organization Uganda(IDLO).

 

Akiongea akiwa kwenye ziara hiyo, Mhe. Owiny-Dollo alisema kuwa  lengo la ziara yao ni kwa ajili ya kubadilishana uzoefu wa jinsi ya kuwandaa Maafisa Mahakama ambao wamepangiwa majukumu mapya na kujifunza jinsi ya kuijengea uwezo Taasisi ya Mafunzo ya Kimahakama ya nchini Uganda (JTI) pia  kujenga ushirikiano katika masuala mbalimbali yanayohusu vyuo na jinsi ya  kuiwezesha Mahakama ya Uganda kufanikisha katika maboresho yake kiutendaji.

Mhe. Owiny-Dollo aliendelea kwa kusema kuwa mafunzo ya kuwandaa Maafisa wa Mahakama wanaopewa majukumu mapya ni muhimu katika kuhakikisha kuwa kunakuwepo huduma bora ya utaoji haki kwa wananchi.

Alisema wanataka kupata uzoefu ambao utawasaidia yeye na ujumbe kutoka Chuo cha Mahakama cha Uganda kuwawezesha watumishi wanaopewa majukumu mapya kupata mafunzo ambayo yatasaidia katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

“Maafisa wa Mahakama walioandaliwa kwa kupewa mafunzo mazuri wataelewa vema majukumu yao na mambo ambayo anatakiwa kufanya katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kupata haki wanapokuwa na mashauri” alisema

Alipokuwa akiwakaribisha wageni hao, Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika alionyesha furaha yake kwa kuushuru ugeni huo kwa kusema kwamba ujio wao ni fursa muhimu ambapo wataitumia kwa kujifunza mambo mbalimbali na kubadilishana uzoefu jinsi vyuo vya Mahakama vinavyofanya kazi.

Naye Mkuu wa Chuo na  Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Dkt. Paul Kihwelo alipokuwa anaelezea historia ya Chuo kilianzishwa kwa Sheria ya Bunge, Sheria Namba 3 ya 1998. Kilianza kazi yake tarehe 23 Oktoba, 2000 na kilikuwa kinatoa Cheti na Diploma ya Kozi za Sheria. Uzinduzi rasmi ulifanywa na Rais Benjamin Mkapa tarehe 3 Agosti 2001.  Pamoja na historia hiyo Mkuu wa Chuo alieleza lengo la madhumuni ya kuanzishwa kwa Chuo ilikuwa ni kujengea uwezo watumishi wa Mahakama.

Ziara hiyo ni sehemu ya ushirikiano kati ya Mahakama ya Tanzania na Mahakama ya Uganda na ujirani mwema kati ya nchi hizi mbili. Sambamba na kutembelea maeneo mbalimbali ya Chuo, Wageni hawa wamepata fursa ya kutembelea maeneo mbalimbali ya vivutio vilivyopo katika Wilaya ya Lushoto.


Jaji Mkuu wa Uganda, Mhe. Alfonse Chigamoy Owiny-Dollo alipokuwa anatoa 
salamu kwa viongozi wa IJA

Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Gerald Ndika 
akitoa neno la ukaribisho kwa Jaji Mkuu wa Uganda na Viongozi wengine wa Mahakama ya Uganda.



Mkuu wa Chuo na  Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe. Dkt. Paul Kihwelo alipokuwa akiwaeleza wageni juu ya historia ya Chuo na shughuli Chuo kinazozifanya

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya JTI Uganda, Mhe. Damilie Lwanga akieleza kwa ufupi shughuli zinazoendeshwa na chuo hicho




Katika picha ni baadhi ya viongozi waliombatana katika Ziara ya Jaji Mkuu wa Uganda wakifuatilia maelezo yaliyokuwa yanatolewa na Uongozi wa IJA kuhusu utendaji kazi wa Chuo
Menejimenti ya IJA wakifuatialia maelezo yaliyokuwa yanawasilishwa na upande wa wageni kutoka Mahakama ya Uganda

Picha ya Mahakimu kutoka Wilaya ya Lushoto wakifuatilia mijadala mbalimbali iliyokuwa inawasilishwa 
Picha ya pamoja ya Jaji Mkuu wa Uganda, Mhe. Alfonse Chigamoy Owinyi- Dollo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe kutoka Uganda.


Picha ya pamoja ya Jaji Mkuu wa Uganda, Mhe. Alfonse Chigamoy Owinyi- Dollo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Menejimienti ya IJA.

Monday, May 23, 2022

IJA YAENDESHA MAFUNZO KWA MAAFISA WA BODI YA SUKARI TANZANIA

Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kimeandaa na kuendesha mafunzo kwa Maafisa 27 kutoka Bodi ya Sukari Tanzania. Washiriki wa mafunzo hayo ni Maafisa wa Bodi ya Sukari Tanzania wa ngazi mbalimbali.  Mafunzo hayo yanafanyika Chuoni Lushoto kwa muda wa siku tano kuanzia tarehe 23 Mei mpaka 27 Mei 2022. 

Akiongea wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo, alielezea lengo la mafunzo hayo  kuwa ni kuwajengea uwezo Maafisa hao kwenye ufafanuzi kuhusu Sheria ya Tasnia ya Sukari, 2002 na Kanuni zake katika kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi. 

Mhe. Dkt. Kihwelo alisema kuwa Mahakama ni chombo cha mwisho katika utoaji wa haki, kwani kuna wadau wengine wa sheria ambao wanafanya kazi hizo za kutoa haki kama Maafisa wa Bodi ya Sukari ambao wajibu wao ni kutoa leseni, kusimamia na kudhibiti soko la sukari nchini. Aliwataka kutumia kile watakachojifunza katika kuongeza ufanisi kwenye utendaji kazi wao ili kupunguza mlundikano wa kesi mahakamani.

Kwa upande wake, Mkuu wa Rasilimali Watu na Utawala, Bw. Linus Bwegoge, alieleza kwamba Bodi ya Sukari Tanzania ina wajibu wa kutoa huduma za udhibiti na kuratibu maendeleo ya Tasnia ya Sukari Tanzania. Aliongeza kuwa ili kutekeleza kwa ufanisi zaidi sheria ya tasnia ya sukari na kanuni zake menejimenti iliona ni vema kuwaleta maafisa wake kwa ajili ya mafunzo hayo. 

Chuo cha IJA kina jukumu la kuwajengea uwezo watumishi wote wa mahakama na mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali yanayotoa huduma za utoaji haki nchini kwa lengo la kuboresha utendaji kazi.  Sambamba na mafunzo hayo Chuo kimebobea katika kufanya mafunzo ya Stashahada na Astashahada ya sheria, kufanya tafIti mbalimbali na  kutoa ushauri wa kitalaamu.


Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo, akifungua mafunzo kwa Maafisa wa Bodi ya Sukari Tanzania 

Naibu Mkuu  Mipango, Fedha na Utawala, Prof. Fatihiya Massawe akitoa neno la ukaribisha kwa  Maafisa wa Bodi ya Sukari Tanzania kwenye mafunzo ya ufafanuzi kuhusu Sheria ya Tasnia ya Sukari, 2002 na Kanuni zake 

Meza Kuu katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo  mafunzo ya ufafanuzi kuhusu Sheria ya Tasnia ya Sukari, 2002 na Kanuni zake 


                         Bi. Zakia Stephano Lwamala,Wakili wa Serikali, Wizara ya Kilimo na mwezeshaji wa  mafunzo ya ufafanuzi kuhusu Sheria ya Tasnia ya Sukari, 2002 na Kanuni zake  akiwasilisha mada kwa washiriki     




Thursday, May 5, 2022

CHUO CHA UONGOZI MAHAKAMA LUSHOTO CHAZINDUA BARAZA JIPYA LA WAFANYAKAZI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Mhe. Mary Makondo ametoa pongezi kwa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kwa kuwa miongoni mwa taasisi chache zinazoongoza nchini kuendesha mafunzo kwa njia ya Mtandao. Ametoa kauli hiyo leo tarehe 5 Mei, 2022 Jijini Dar es Salaam katika Taasisi ya Mafunzo ya Sheria kwa Vitendo katika hafla ya uzinduzi wa Baraza la Nne la Chuo ambapo amesema Chuo kimekuwa kikifanya vizuri kwenye eneo la mafunzo kwa njia ya mtandao sio tu nchini bali pia katika ukanda wa Afrika na nje ya mipaka ya Afrika. 

Mhe. Makondo alieleza kwamba katika kipindi hiki cha Mapinduzi ya Nne ya Viwanda ambapo matumizi ya TEHAMA na Akili Bandia yamezidi kushika kasi, hali hiyo imetokana na ukweli kuwa Mahakama ya Tanzania ni Mhimili unaofanya vizuri kwenye matumizi ya TEHAMA katika utendaji kazi wa kila siku ikiwemo uendeshaji wa mashauri. 

 Aliendelea kusema kuwa Chuo kama wakala wa mafunzo kwa kutumia TEHAMA kupitia mfumo wa virtualcourt umeweza kuendesha mafunzo kwa zaidi ya watumishi 1500 wa mahakama ya Tanzania mpaka sasa na idadi hiyo inaendelea kuongezeka. Amesema njia hiyo imeweza kukisaidia Chuo kuwafikia watumishi wa Mahakama popote walipo bila usumbufu wa kusafiri ambapo njia hiyo imeweza kupunguza gharama za kuwalipa watumishi kwa ajili ya kuhudhuria mafunzo mbalimbali.

Mhe.Makondo ameonyesha  kufarijika kwa jitihada zinazofanywa na chuo cha uongozi wa mahakama Lushoto kwa kuendesha  mafunzo mbalimbali kwa kutumia mifumo ya Tehama iliyotengenezwa na wataalamu wa ndani .

"Nimefarijika sana kuona chuo kimetumia mfumo uliojengwa na watalaamu wetu badala ya kutumia mifumo kama Microft teams , zoom hii inatuhakikishia usalama wa mifumo pamoja na kujenga uwezo wa ndani ,nitoe rai kwa chuo kuharakisha kuanzisha mafunzo ya muda mfupi ya komputa kwa wanasheria" alisema Makondo.

 Aidha Mhe.Makondo amewataka wajumbe walioteuliwa katika Baraza la wafanya kazi kuhakikisha wanakuwa mabalozi wazuri kwa wafanyakazi wanaowawakilishi na siyo kuwa mizigo kwa uongozi na wafanyakazi katika kutatua kero zao.

 Aidha Mhe. Makondo ameupongeza uongozi wa Chuo kwa jitihada za kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kununua viwanja jijini Mwanza na Mkoani Simiyu na kusema kufanya hivyo ni hatua kubwa kwa Chuo. "Wizara inaamini kwamba uendelezaji wa viwanja hivyo utafanyika kwa haraka ili kufikisha huduma karibu na wananchi kama ilivyokusudiwa,"alisema.

Mhe. Makondo ameahidi kuwa Wizara anayoiongoza iko tayari kutoa ushirikiano unaostahili kwa Chuo wakati wowote watakapouhitaji.

Mhe. Makondo àlitumia hafla hiyo kutoa wito kwa waajiri wote wanaoajiri wanasheria katika utumishi wa umma kuwapeleka watumishi hao kupata mafunzo katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kwa mujibu wa matakwa ya Waraka wa Katibu Mkuu Ofisi ya Raisi Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Waraka Namba 5 wa mwaka 2012. 

Kwa upande wake Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi  Mhe.Dkt. Paul Kihwelo amesema kuwa kwa kanuni ya 108 ya sheria za utumishi wa umma 2003 kanuni zinaelekeza kuwepo kwa chombo ambacho kitahakikisha kuwepo kwa mahusiano mazuri kazini pamoja na kuhakisha masilahi ya watumishi yanazingatiwa kwa mjibu wa sheria.

Mhe. Dkt. Kihwelo aliendelea kusema kuwa wajibu wa Chuo ni kuwajengea uwezo watumishi wa mahakama kwa kada mbalimbali Tanzania ili kuboresha utendaji wa kazi kwa maafisa. 

Hafla hiyo ya uzinduzi ilikamilika kwa wajumbe kupewa mafunzo ya siku moja ya Haki na Wajibu wa Mtumishi wa Umma pamoja na Maadili ya Utumishi wa Umma mafunzo ambayo yameendeshwa na wawezeshaji wabobezi kutoka Ofisi ya Raisi Menejimenti ya Utumishi ya Umma.

Lengo la mafunzo hayo ni kuleta tija kwa watumishi, taasisi na taifa ili kuweza kukabiliana na changamoto zitakazojitokeza katika utumishi wa mma kwa kuwa Baraza la wafanyakazi ni kioo na mwanga wa taasisi. 


Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Mhe. Mary Makondo akiongea na Wajumbe wa Baraza Jipya la Wafanyakazi la Chuo cha Uongozi wa Mahakama wakati wa uzinduzi wa Baraza hilo.





Picha mbalimbali za  Wajumbe wa Baraza Jipya la Wafanyakazi la Chuo cha Uongozi wa Mahakama wakiwa wanafuatilia hotuba wakati wa hafla ya uzinduzi wa Baraza.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Mhe. Mary Makondo akipokea zawadi ya Tisheti kutoka kwa Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi  Mhe. Dkt. Paul Kihwelo katika hafla ya uzinduzi wa Baraza la Nne la Chuo

Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Mhe. Mary Makondo akipokea zawadi kutoka kwa Mhe. Dr. Benhajj S. Masoud, Jaji wa Mahakama Kuu na Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Sheria kwa Vitendo katika hafla ya uzinduzi wa Baraza la Nne la Chuo


Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto na Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi  Mhe. Dkt. Paul Kihwelo akipokea zawadi kutoka kwa Mhe. Dr. Benhajj S. Masoud, Jaji wa Mahakama Kuu na Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Sheria kwa Vitendo  katika hafla ya uzinduzi wa Baraza la Nne la Chuo