Na: Rosena Suka IJA Lushoto
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria wamefanya ziara ya kukagua mradi wa ujenzi wa bweni la ghorofa nne la wavulana lenye thamani ya shilingi za kitanzania billioni 2.64 lenye uwezo wa kulaza wanachuo 320. Mradi huu unasimamiwa na Mahakama ya Tanzania katika mpango wa Maboresho ya Mahakama.
Akizungumza wakati wa ukaguzi wa jengo hilo la bweni la wavulana Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel ametoa ufafanuzi wa ujenzi wa jengo hilo kuwa umefanyika katika awamu tatu tofauti ambazo zilisimamiwa na wakandarasi watu watatu kwa nyakati tofauti toka kuanza kwa mradi wa ujenzi huo mwaka 2011.
Prof. Elisante alitoa maelezo
hayo kwa kusema kuwa awamu ya kwanza ya mradi huo ilikuwa chini ya mkandarasi Beijini Construction Engineering Group ambaye
alijenga kuanzia msingi hadi boma. Hatua ya pili ilikuwa ni uwekaji wa mifumo
mbalimbli katika jengo hilo chini ya usimamizi wa Mkandarasi Froton Afrika Limited na Mkandarasi aliyepo kwa sasa ni MS-Works
Construction Limited ambaye anaendelea na umaliziaji wa jengo hilo ambalo litakapokamilika litakuwa na miundombinu ambayo itawezesha wanafunzi
kutoka katika makundi maalum kulitumia.
Pamoja na mengine Prof.
Elisante alimalizia kwa kusema kuwa, jengo hilo litakabidhiwa ifikapo Mei, 2022
na linatarajiwa kutumiwa na wanachuo watakaosajiliwa katika mwaka wa masomo
2022/2023 ambapo litapunguza idadi kubwa ya wanachuo wakiume wanaoishi nje ya
mazingira ya Chuo.
Kaimu Mwenyekiti wa
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la
Tabora Mjini Mhe. Emmanuel Mwakasaka ameipongeza Serikali kwa hatua iliyofikia
ya ukamilishwaji wa ujenzi wa Jengo la Bweni la Wavulana la Chuo cha Uongozi wa
Mahakama. Hatua ya ujenzi wa bweni hili litakuwa ni mkombozi kwa Chuo kwani litawezesha
wanachuo kuweza kuishi ndani ya chuo badala ya kuchanganyika na wenyeji.
“Miradi ya ujenzi wa
majengo haya imeenda kwa haraka sana na tumeridhishwa sana na kazi
iliyofanyika, pongezi kwa watendaji wote wa Mahakama”, alisema Mhe. Mwakasaka.
Naye, Naibu Waziri, Wizara ya Katiba
na Sheria Mhe. Geogrey Pinda (MB) alishukuru Kamati ya Kudumu
ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa kutembelea mradi
huo na kuahidi kuwa hoja zote zilizotolewa na wajumbe zimepokelewa na
zitafanyiwa kazi. Mhe. Pinda pia alitoa mapendekezo kwa Chuo kutumia nafasi
waliyonayo kuendelea kuwajengea uwezo watumishi wa mahakama ili kusaidia
mabadiliko ya mahakama kwenda sambamba na wataalamu.
Kwa upande
wake Naibu Mkuu wa Chuo Taaluma, Tafiti na Ushauri Bw. Goodluck Chuwa ameipongeza
Mahakama ya Tanzania kwa kutoa ushirikiano mkubwa kwa Chuo kwa kukiwezesha mafunzo
ya kuwajengea uwezo watumishi wa kada mbalimbali wa Mahakama pamoja na wadau wa
sheria nchini.
Kamati
ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria imefanya ziara ya siku moja ambapo imekagua mradi wa ujenzi
wa jengo la bweni la wavulana la Chuo cha Uongozi Mahakama Lushoto ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya
kamati hiyo ikiwemo kufanya ukaguzi wa miradi ya ujenzi inayosimamiwa na
Mahakama ya Tanzania.
(Picha na Ibrahim Mdachi - IJA Lushoto)






0 comments:
Post a Comment