Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

Wednesday, August 31, 2022

JAJI MKUU WA TANZANIA ASISITIZA MAADILI KWA MAJAJI

 Na Rosena Suka IJA

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma jana tarehe 30 Agosti, 2022 alifungua mafunzo elekezi yanayowaleta pamoja Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wapya 21 na wengine wanne wa Mahakama Kuu Zanzibar ambapo amewahimiza kuzingatia maadili wanapotekeleza majukumu yao ya utoaji haki kwa wananchi.

Mhe. Prof. Juma aliwataka Majaji hao kusoma na kujadili miongoni mwao Kanuni za Maadili za Maafisa Mahakama iliyochapishwa tarehe 20 Novemba, 2020 kupitia Tangazo la Serikali Namba 1001 la mwaka 2020 ambazo zitawasaidia kubaki ndani ya matarajio ya kimaadili.

“Uwezo na Maadili ni nguzomuhimu ya kuaminiwa na kuaminika kwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania. Uwezo, Ujuzi na Maarifa yenu yatajenga Imani na kuaminiwa kwenu kwa namna ambavyo mtafanya maamuzi yenu kwa haki, kwa kuzingatia Katiba, Sheria, Kanuni, Taratibu, Miongozo, Mila na Desturi za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema.

Jaji Mkuu akawakumbusha kuwa pamoja na maadili ya Viongozi wa Umma; Majaji wa Mahakama Kuu, Majaji wa Rufani, Wasajili, Mahakimu, na Wasaidizi wote wa Majaji, wanaongozwa na Kanuni za Maadili za Maafisa wa Mahakama (Code of Conduct and Ethics for Judicial Officers, 2020).

Amesema uongozi wa Mahakama ukishirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), umeweka utaratibu wa Mafunzo elekezi ya awali kwa wote walioapishwa kuwa Majaji wakiwemo wale wanaojiunga na utumishi wa Mahakama kwa mara ya kwanza.

“Mafunzo elekezi yanalenga kuwatayarisha kutumikia nafasi ya Jaji. Mafunzo elekezi yanawakaribisha rasmi katika Utumishi wa Mahakama wenye maudhui, tamaduni, mitizamo na uzoefu uliojengeka muda mrefu ambazo itawawekea misingi imara ya kuwasaidia katika utoaji wa huduma za kimahakama,” amesema.

Jaji Mkuu amebainisha pia kuwa mafunzo hayo elekezi yanalenga kuwajengea msingi wa kuifahamu Mahakama, kufahamu mwelekeo wa Mhimili wa Mahakama ndani ya maudhui ya mwelekeo wa nchi ya Tanzania ndani dunia inayoizunguka.

Akaseama kuwa kwa upande wake Mhimili wa Mahakama utafaidika na uwezo, uzoefu, ujuzi na umahiri wa Majaji hao waliojijengea kutoka maeneo waliyopitia, hivyo mchanganyiko huo utakuwa wa faida kubwa kwao binafsi, kwa Mahakama na pia kwa pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Jambo moja muhimu ambalo litajitokeza katika Mafunzo haya elekezi ni dhamira dhahiri ya Mahakama ya Tanzania kuwaingiza kuwa sehemu ya waboreshaji wa huduma za utoaji haki kupitia Mipango Mkakati na Programu za Maboresho,” Mhe. Prof. Juma alisema.

Amesema kuwa Maboresho ya Mahakama yanayoendelea hivi sasa yamewajengea watumishi wa Mahakama utamaduni mpya, mitazamo mipya na mwelekeo mpya wa utoaji wa huduma za haki kwa kumlenga na kumridhisha mwananchi (Citizen-Centric Judicial Modernization and Justice Service Delivery).

“Ninawasihi muwe sehemu ya dhana hii ya utoaji wa huduma za haki kwa kumlenga na kumridhisha mwananchi. Mafunzo haya elekezi yanawatayarisha Majaji wapya kuifahamu Dira ya Mahakama ya Tanzania—Timely and Accessible Justice for All,” Jaji Mkuu alisema.

Aidha, Mhe. Prof. Juma akabainisha kuwa katika kumlenga na kumridhisha mwananchi, Jaji sio idadi bali umuhimu wake kwa mwananchi ni huduma bora za haki, ujuzi, ufanisi, na uwazi wa huduma za utoaji haki kwani wananchi wanafuata huduma mahakamani, wala hawaji kumtembelea Jaji, wanafuata huduma za utoaji haki.

Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Juma  akifungua Mafunzo Elekezi kwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mahakama Kuu Zanzibar uliofanyika tarehe 30 Agosti, 2022 katika Ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto,(IJA)  Mhe. Dkt. Gerald Ndika na kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe Mustapher Siyani






Picha ya chini na ya juu ni Sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mahakama Kuu ya Zanzibar wakimsikiliza Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani)


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mahakama Kuu ya Zanzibar mara baada ya kufungua mafunzo elekezi. Wengine walioketi mbele ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe Mustapher Siyani (wa tatu kulia),Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi la Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Gerald Ndika (wa tatu kushoto), Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Faustine Kihwelo (wa pili kushoto), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Mhe. Gerson Mdemu (wa pili kulia), Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Dkt. Eliezer Mbuki Feleshi (wa kwanza kushoto) na Mjumbe wa Tume ya Utumishi wa Mahakama Wakili Genoveva Katto.



Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji Wanawake wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mahakama Kuu ya Zanzibar mara baada ya kufungua mafunzo elekezi kwa Majaji.

0 comments:

Post a Comment