Drop Down MenusCSS Drop Down MenuPure CSS Dropdown Menu

Friday, November 24, 2023

IJA NI TANURI LINALOPIKA WAHITIMU BORA

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amekipongeza Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kwa kutoa wahitimu waliopikwa katika tanuri la vielelezo vya ubora  na ufanisi wa huduma kwakuwa na uwezo wa kukabiliana na kumudu mabadiliko yoyote katika soko la ajira. Rai hiyo aliitoa leo tarehe 24 Novemba, 2023 wakati wa mahafali ya 23 kwa wahitimu 831 wa ngazi mbalimbali wa  Chuo Cha Uongozi wa Mahakama yaliyofanyika Chuoni Lushoto.

Alisema kuwa kufanyika kwa mahafali ya Chuo ni uthibitisho wa mafanikio makubwa kwa Wanafunzi waliohitimu kupitia juhudi kubwa za Uongozi wa Chuo na wanataaluma. Aliendelea kwa kusema mahafali ni wakati mzuri wa kujitathmini na kutambua kuwa Chuo chetu kimepiga  hatua kubwa katika kutoa elimu bora, Mafunzo Endelevu ya kimahakama, kufanya tafiti na  ushauri elekezi kwa kushirikiana na wadau mbali mbali wa sheria wa  ndani na nje ya nchi. Mahakama ya Tanzania imekuwa ikivunia kuwa na Chuo chenye kutekeleza malengo yaliyokusudiwa.

Aidha,  Mhe. Prof. Juma aliwakumbusha wahitimu kuwa ni muhimu kufahamu vyema mabadiliko ya kiuchumi, kijamii na kisiasa yanayogusa Tanzania na Dunia kwenye matumizi ya Tecknolojia ya Habari na Mawasiliano yanayosukumwa na Akili Bandia ambayo yamefanya mabadiliko katika utoaji wa huduma kwa kutumia teknolojia za kisasa.

“Tahadhari muhimu hapa, kila mmoja wenu anatakiwa kubadilika na kujiongezea ujuzi na umahiri katika matumizi ya teknolojia katika kutoa huduma. Uwezo uliotokana na Astashahada ya Sheria (Certificate), na Stashahada ya Sheria (Diploma in Law) peke yake hautakuwezesha kupata ajira za kiushindani katika Tanzania na Dunia ya Dijitali” alisema Mhe. Prof. Juma.

Pamoja na hayo Mhe. Prof. Juma amefarijika kwa kuona Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto umefikia hatua nzuri ya kukamilisha ujenzi wa jukwaa la ufundishaji wa elimu kwa njia ya ki-elekitroniki (E-LEARNING PLATFORM).  Akaendelea kwa kutaja faida kadhaa zitakazotokana na ufundishaji wa njia hiyo ya ki-elekitroniki ni pamoja na kuwafanya wanafunzi kuhudhuria masomo yao huko huko waliko  huku wakiendelea na kazi zao.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Dkt. Gerald Ndika alisema Chuo kimepata mafanikio makubwa kwenye  kutoa Mafunzo, warsha na makongamano mbalimbali. Pamoja na mafunzo na makongamano yanayofanywa Chuo pia kinafanya tafiti mbalimbali kukidhi mahitaji ya  kuwajengea uwezo wataalamu wetu. Tafiti hizo zimepelekea Chuo kuandaa machapisho mbalimbali kama vile kitabu cha mkusanyiko wa maamuzi ya Mahakama kuhusu unyanyasaji na ukatili wa kingono kwa watoto.  Hii inadhihirisha waziwazi Chuo kinavyoshirikiana na jamii dhidi ya kupinga unyanyasi na kulinda na kutetea haki ya mtoto.

Mhe. Dkt Ndika aliendelea kwa kumhakikishia  Jaji Mkuu wa Tanzania kuwa Chuo kiko kwenye maandalizi ya kufatilia huduma zinaofanywa na wahitimu wake katika maeneo mbalimbali kwa kufanya tathimini mahususi.  Hii imetokana na wahitimu wa Chuo kuhitajika katika maeneo mbalimbali.

Naye Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo, Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo katika maelezo yake alimshukuru Mhe Dr. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mnamo tarehe 20 Septemba 2023 kuridhia mapendekezo ya Kamati ya Raisi ya Utekelezaji (PIC) na kuidhinisha Muundo wa Mgawanyo wa Majukumu ya Chuo ili kuimarisha utendaji kazi.  Katika muundo huo umeanzisha Kurugenzi ya Mafunzo ya Kimahakama na Elimu Endelevu ambayo jukumu lake kubwa litakuwa ni  kuratibu mafunzo ya Kimahakama kwa maafisa wa Mahakama na watumishi wengine wa Mahakama na wadau mbalimbali wa sekta ya sheria nchini.

Jumla ya wanachuo 851 wamehitimu masomo yao ambapo Astashahada ya Msingi ya Sheria (Basic Technician Certificate in Law) jumla ya wahitimu ni 336 ambapo wakike ni 177 na wakiume ni 159, Astashahada ya Sheria (Technician Certificate in Law) jumla ya wahitimu ni 242 ambapo wakike ni 101 na wa kiume ni 141 na kwa upande wa Stashada ya Sheria (Diploma in Law) jumla ya wahitimu ni 273 ambapo wakike ni 137 na wa kiume ni 136. 












0 comments:

Post a Comment